Wednesday, February 29, 2012

KWA NINI WASICHANA HUBABAIKIA WENYE MAGARI NA FEDHA?


Inasemekana wasichana wa mijini wanadanganyika zaidi kwa magari. Msichana anakubali kuwa na uhusianao na mwanume kwa sababu amegundua kwamba ana gari, hata kama anajua kwamba hilo gari sio la huyo mwanaume, lakini hujikuta akikubali kuwa na uhusiano na mwanaume huyo kwa sababu ya gari tu.

Ndio maana madereva wengi hasa wale wa teksi wanajisifu kwamba wanawake wanawapapatikia sana.

Je hili lina ukweli kiasi gani?

Lakini je ni wasichana wote ambao wanawapapatikia madereve au watu wenye magari?
Nadhani hili ndilo swali gumu sana kwenye suala hili
Kila kitu kinachohusu uhusianao wa kimapenzi, tunajifunza kutoka kwa wazazi au walezi wetu, labda asilimia 10 tu ndio tunayojifunza nje ya nyumbani.

Siyo suala la gari peke yake, bali ni suala la karibu kila kitu. Je watoto wetu tunawajengea dhana gani kuhusu kila kitu kwenye maisha?
Halafu tunawaambia kitu gani kuhusu kupenda?
Siku zote na tulio wengi tunawaambia watoto wetu uongo mwingi sana, na uongo huo unatokana na sababu nyingi.
Kwanza nasi tulidanganywa na wazazi wetu. Pili hatujiamini. Tatu hatuna uhakika sisi ni akina nani, na nne tunadhani uongo huo utawasaidia watoto wetu.
Hebu chunguza kwa makini utagundua kwamba, wasichana wanaobabaikia magari ni wale ambao wamelelewa kwenye malezi ya uongo mtupu.

Unaweza kudhani wale waliotoka kwenye familia masikini ndiyo ambao wanababaikia magari, hapana.
Msichana anaweza kutoka kwenye familia masikini na asibabaikie utajiri wala magari, wako wengi wa aina hiyo.
Kama nyumbani wazazi wanawasifu wenye magari, wanaonesha kwamba ukiwa na gari ndio unakuwa na maana, kwamba ndio kiwango cha juu cha mafanikio, unatarajia kitu gani kutoka kwa watoto?
Kuna wakati wazazi wanasema , “ameshafika mbali sio mwenzio, yule ana akili sana. Ana magari mawili na nyumba tatu.

Wakati mwingine inatosha mara moja tu, jambo kusemwa na mzazi, na mtoto kuamini kwamba mwenye gari au magari na nyumba ndiye aliyekamilika, ndiye mwenye akili..

Kumbuka mtoto anaingiza maarifa akilini mwake kutoka kwa watu anaowaamini anaokutana nao maishani. Kwenye suala la uhusianao wazazi ndio wanaoaminika zaidi.

Kwa sababu ya umasikini wetu, tulio wengi na uhaba wa malengo makubwa kuliko sisi wenyewe, gari na nyumba ndio malengo ya juu kabisa ya binadamu kuyapata.

Mtoto anakuwa na akili ya aina hiyo, kigezo chake kuhusiana na mtu kitakuwa ni gari, nyumba au mali kwa ujumla.
Kwake binadamu mwenye maana na anayefaa ni yule anayemudu kumiliki vitu hivyo.

Hii sio kwa wasichana peke yake bali hata wanaume. Kama mtoto wa kiume alioneshwa kuwa thamani ya mtu inatoka kwenye gari, nyumba na mali, basi naye atakuwa anababaikia vitu hivyo.

Linapokuja swala la uhusianao, atajitahidi kumuonesha msichana kwamba anavyo vitu hivyo au anao uwezo wa kuvimiliki. Anafanya hivyo kwa sababu aliambiwa thamani yake inakuwepo pale anapokuwa na vitu hivyo.

Wazazi wengi wameegemeza thamani zao kwenye vitu badala ya wao wenyewe. Bila ya hiyari yao wanawafundisha watoto wao kujali na kuthamini vitu badala ya utu wao.
Kwa kadiri mfumo wa maisha wa mitaji ulivyokuwa ukiendelea, binadamu alijitoa thamani na kuiweka kwenye vitu, hasa mali.

Kwa bahati mbaya wale watoto wa wazazi ambao wana maisha ya kati ndio ambao wanasumbuliwa na mali.

Kwa nini?

Kwa sababu wazazi wao hawajui kama wako juu au chini kimapato.

Katika kujitafuta hutoa kauli zenye kuonesha kwamba maisha ni mali, basi.

Wazazi walio na kipato cha chini nao wanaweza kuwaathiri vibaya watoto wao, kwa kuzungumza na kutenda katika njia ambayo watoto wataamini kwamba umasikini huondoa kabisa thamani ya mtu.Wale walio juu kabisa wanaweza wasifikirie kwamba gari au nyumba ni mambo ya maana sana, hata kama wamefundishwa kuhusu mali. Wao watafikiria mali kwa mkabala mkubwa zaidi.

Labda watafikiria kuhusu ndege au kutembelea boti ya kifahari na mengine, lakini wote watakuwa na udhaifu ule ule wa kuamini kwamba mali ni kubwa kuliko thamani ya binadamu.
Mali ambayo unaitengeneza na kuitafuta mwenyewe halafu iwe kubwa kuliko wewe! Hii ni ajabu kabisa.

Wazazi ambao wanachukulia mali kama kitu cha kawaida sana, ambacho uwe nacho au usiwe nacho, maana ya maisha haibadiliki, na thamani yako haiondoki kamwe, hawa ndio watoto wao watakuwa na maisha bora.

No comments:

Post a Comment