Friday, February 17, 2012

MJUE CHE GUEVARA

Che guevara
Ernesto Rafael Guevara de la Serna au Che Guevara kuzaliwa  (* 14. Mei 1928 Rosario, Argentina; kifo † 9. Oktoba 1967 La Higuera, Bolivia) alikuwa mtabibu mzaliwa wa Argentina aliyekuwa mfuasi wa itikadi za Kisoshalisti za Karl Marx. Guevara anajulikana zaidi kwa harakati zake za kimapinduzi dhidi ya tawala za kibepari huko Amerika ya Kusini na Afrika.
Wakati akisomea utabibu, Che Guevara alizunguka katika nchi mbalimbali za Marekani ya Kusini ambapo alijionea mwenyewe umasikini uliokithiri. Alisikitishwa sana na maisha ya ufukara waliokuwa wakiishi wananchi wengi huku wachache wakiwa wanamiliki mali za nchi hizo. Alifikiria jinsi ya kuweza kubadili hali hii na kuamua kuwa njia pekee ya kuondoa umasikini na ukandamizaji ni mapinduzi. Aliamua kusoma kwa undani falsafa za Karl Marx na baada ya hapo alijihusisha na harakati za kisoshalisti nchini Guatemala chini ya rais Jacobo Arbenzi Guzmán.
Mwisho mwa miaka ya 1950, Guevara aliungana na Fidel Castro aliyekuwa akiongoza kundi la kijeshi lililotwaa madaraka kwa nguvu nchini Kuba mwaka 1959. Guevara alikuwa mmoja wa viongozi wa serikali mpya ya Kuba. Katika kipindi hiki, Guevara aliandika vitabu na makala mbalimbali kuhusu nadharia na vitendo vya vita vya msituni kwa nia ya kuondoa madarakani tawala za kibepari na kibeberu.
Mwaka 1965 Guevara aliondoka nchini Cuba akielekea Kongo-Kinshasa (hivi sasa inaitwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo) kwa siri kusaidia harakati za kuondoa utawala uliokuwa ukiongozwa na vibaraka wa mataifa ya Magharibi chini ya Mobutu Sese Seko baada ya kuuawa kwa Patrice Lumumba. Moja ya watu ambao walifanya kazi na Guevara alipokuwa nchini Kongo ni aliyekuwa baadaya rais wa nchi hiyo, Laurent Kabila.
Guevara aliondoka nchini Congo na kuelekea Bolivia ambapo alikamatwa mwaka 1967 na jeshi la Bolivia likishirikiana na majasusi wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA). Baada ya kukamatwa kwake aliuawa kinyama.
Baada ya kifo chake, Guevara alichukuliwa kama nguzo ya vuguvugu la kimapinduzi ya kishoshalisti duniani. Picha yake na kofia aina ya Beret aliyopenda kuivaa vimekuwa kama alama za mapinduzi ya mrengo wa kushoto duniani

No comments:

Post a Comment